TENGENEZA BLOG BOMBA SASA..

Obama kuiangalia Iran kwa muelekeo gani?

Rais Barack Obama wa Marekani amesema anaamini kwamba makubaliano ya nyuklia kati ya Iran na nchi zinazounda kundi la 5+1 yameandaa mazingira ya kuboreshwa uhusiano kati ya Washington na Tehran. Akizungumza juzi Jumamosi katika mahojiano aliyofanyiwa na kanali ya televisheni ya CNN, Obama alisema makubaliano ya nyuklia yanaandaa mazingira ya kufikiwa lengo kuu ambalo ni kuboreshwa uhusiano baina ya Washington na Tehran.
Hadi sasa, Marekani imepoteza fursa nyingi za kuboresha uhusiano na Iran; hivyo kuzungumzia maelewano ya siku za usoni kati ya Marekani na Iran, hata kama ni kwa kwango cha utoaji kauli tu kungali mbali mno na uhalisia wa mambo. Masuala mengi machungu bado yangaliko ambayo wingu lake jeusi lingali limetanda kwa miaka na miaka sasa kwenye anga ya uhusiano wa Iran na Marekani. Obama anadai kwamba nia yake si kuwa na uadui na Iran, lakini katika kutetea kwake makubaliano ya nyuklia angali ameshikilia madai kuwa Iran ni tishio, na kwamba hatua ijayo atakayochukua katika Mashariki ya Kati ni kupunguza kile alichodai, wasiwasi unaotokana na siasa za Iran katika eneo hili. Marekani inawapa ahadi waitifaki wake wa jadi na majirani wa Iran kuwa itaendelea kuwauzia silaha za mabilioni ya dola ili eti kuwafanya wawe imara kukabiliana na vitisho vya Iran, hatua ambayo ni ya kuchochea mifarakano kati ya nchi za eneo na kueneza sumu ya hali ya kutoaminiana baina yao. Katika sehemu nyengine ya mahojiano hayo aliyofanyiwa na CNN, Rais wa Marekani alisema pia kama ninavyomnukuu:”Sisi tumefanya mazungumzo na utawala unaopiga nara za ‘mauti kwa Marekani’; hata hivyo hakusema ni kwa nini wananchi wa Iran wanapiga nara na sha’ar hizo. Ili kuelewa chanzo na sababu ya hatua za kiadui za Marekani dhidi ya Iran, inafaa tuuangazie mwenendo wa Washington, si katika kipindi cha miongo mitatu tu nyuma, bali kwa kipindi chote cha nusu karne iliyopita. Hatua za kiadui za Marekani dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran hazijakomea kwenye mapinduzi ya kijeshi au vitendo vya ujasusi tu vilivyokuwa vikifanywa na ubalozi wa nchi hiyo hapa mjini Tehran. Katika hatua yake ya kwanza mara baada ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu, Marekani ilichukua uamuzi wa kiadui kwa kuzuia fedha na mali za Iran zilizokuweko katika mabenki ya nchi hiyo na hivyo kuanzisha rasmi kampeni ya kuliwekea mzingiro wa kiuchumi taifa hili na kutaka litengwe; na katika kipindi cha miaka yote iliyopita baada ya hapo imechukua hatua kadha wa kadha kwa lengo la kuvuruga uthabiti ndani ya Iran. Jaribio la uvamizi wa kijeshi la mwezi Aprili mwaka 1981 katika jangwa la Tabas mashariki mwa Iran na kuuunga mkono utawala wa Saddam katika vita vya miaka minane ulivyoanzisha dhidi ya Iran, yote hayo yalifanyika kwa lengo hilo. Shambulio la mwezi Julai mwaka 1988 la kombora la manuwari ya Marekani ya USS Vincennes, lililoitungua kwa makusudi ndege ya abiria ya Iran ni jinai nyengine iliyofanywa na Washington na kusababisha vifo vya abiria 290 waliokuwemo ndani ya ndege hiyo iliyokuwa ikitoka Bandar Abbas kuelekea Dubai. Misimamo na harakati zote hizo za kiadui ni kumbukumbu za faili chafu la nusu karne ya uingiliaji na uadui wa Marekani dhidi ya taifa la Iran, kumbukumbu ambazo haziwezi kufutika katu ndani ya fikra za Wairani na historia ya nchi yao. Japokuwa hivi sasa Obama anajaribu kuonyesha kuwa mwenendo wake yeye ni tofauti na watangulizi wake, lakini kivitendo amethibitisha kuwa mtazamo wake juu ya Iran hauna tofauti ya kiasi hicho kulinganisha na waliomtangulia. Ndiyo kusema kuwa dhana na utabiri juu ya uhusiano wa Marekani na Iran baada ya makubaliano ya nyuklia unategemea mambo mengi ambayo wakati ndio utakaohukumu juu yake. Na kwa hivyo katika kipindi hiki cha sasa mazungumzo kati ya Iran na Marekani yamefanyika kuhusiana na kadhia ya nyuklia tu, si zaidi ya hilo. Na mtazamo wa Iran juu ya Marekani utaweza kubadilika pale yatakaposhuhudiwa mabadiliko ya kweli katika mwenendo na muamala wa Washington…/
Share on Google Plus

About NELSON PASCHAL KAMUGISHA

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

CREATED AND DESIGNED BY NELLYPAKA(WWW.NELLYPAKA.BLOGSPOT.COM)