Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limelaani vikali hujuma ya
kigaidi iliyotokea jana Jumamosi kwenye mji mkuu wa Mali, Bamako,
ambapo watu 5 walifariki dunia na wengine kujeruhiwa. Miongoni mwa
majeraha ni wafanyakazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa kuhusu mabomu
yaliyotegwa ardhini UNMAS, Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Mali
MINUSMA na Muungano wa Ulaya.Wanachama wa Baraza la Usalama wamepeleka salamu zao za rambirambi kwa familia za wahanga na serikali za Mali, Ufaransa na Ubelgiji, pamoja na kuwatakia nafuu waliojeruhiwa. Aidha wanachama wa baraza la Usalama wameiomba serikali ya Mali ipeleke watekelezaji wa uhalifu huo mbele ya sheria haraka iwezekanavyo. Halikadhalika, wakilaani aina zote za vitendo vya ugaidi, wamesisitiza umuhimu wa kupambana navyo kwa kuheshimu haki za binadamu. Afisa mwandamizi wa usalama amesema watu wawili waliokuwa wamebeba silaha ndio waliofanya shambulio hilo, ambapo mmoja alivamia mkahawa wa La Terrasse na kuwafyatulia watu risasi kisha kupanda gari lililokuwa likiendeshwa na mwenzake aliyekuwa akimngojea nje ya mkahawa huo.



0 comments:
Post a Comment